Mama Mjata na Kisa cha Kifo Bandia (kutoka R.I.P. mpaka L.I.P.)




Ni siku nyingine mpya katika mji huu wa Bagamoyo, Mji wenye utajiri wa historia ya kale, watumwa na kisima cha zamani kisichokauka maji, magofu pamoja na hoteli za kisasa zilizojengwa katika kipindi hiki na kuufanya mji kupata sura mpya lakini bado ule ukale uanaowavutia wazungu wengi kuja kutalii bado unaonekana.

Bagamoyo ni mji ulio kandokando ya bahari ya Hindi, bahari iliyopambwa na mikoko ukingoni mwake na pia chuo pekee cha sanaa mjini hapa TASUBA ni kimbilio la wasanii wengi toka mikoa mbalimbali ya nchini Tanzania.

Huwa ninaendaga mara nyingi kumtembelea mtoto wangu anaeishi hapa na kama kawaida  ya siku nyingine zote, niliamshwa asubuhi na mwanga uliopenya kupitia pazia zuri na jepesi lililowekwa dirishani huku kiupepo chepesi kikinipiga na kunifanya nihisi baridi flani hivii...kitu ambacho sio cha kawaida, maana kila siku huwa nakifurahia hiki kiupepo lakini nashang’aa leo nahisi baridi!   Mmh!?   Kuna jambo!

Niliamka pale kitandani na kuhisi maumivu katika viungo na mwili haukuwa katika hali yake ya kawaida. nilitoka nje baada ya taratibu za usafi na kumsalimia mwanangu Anita na kumweleza kinachonisibu.
“najihisi naumwa, sijui ni nini.. lakini aah, tuache tu  hii hali itapita”
Anita hakukubali, aling’ang’ania uamuzi wake wa kunipeleka hospitali na hatimae ilinibidi nikubali na kwa pamoja tuliongozana wote hadi kwa daktari ambae aliponiona tu alisema.
“mama  mjata si wiki iliyopita  tu tulipima malaria na ukawa huna? lakini sio mbaya tukipima tena”
Nilienda kupima na kukutwa na malaria ambayo kwa umri kama wangu huwa inaambatana na shoga yake presha!  Nikalazwa.

Nilipofika wodini na kupewa kitanda nilishangazwa na sauti ya mkoromo uliosikika hivyo nikaanza kuangalia majirani zangu upande huu na ule na kumwona bi mkubwa mmoja akiwa katika hali mbaya ndie anaesababisha mkoromo huo! sikuweza kwenda kumwangalia kwa vile nilishatundikiwa dripu hivyo nikawa naishia kumsikiliza huku nikimwombea kimya kimya.
Anita ilibidi arudi nyumbani kwa ajili ya kuandaa chakula maana nilikuwa na njaa sana na daktari alishauri nipate chakula kutokana na madawa ninayotumia, hivyo nikabaki peke yangu nikiiangalia dripu inavyoteremka tone baada ya tone.

Kawadia ya mfanyakazi yeyote anapopatwa na tatizo kama hili la kuuguliwa inabidi arudi kazini na kuomba ruhusa au kutoa taarifa kuwa hatakuwepo kwa muda akamhudumie mgonjwa kisha atarudi, na ndivyo alivyofanya Anita na baada ya kupewa ruhusa alirudi nyumbani na kuanza kazi ya kuandaa chakula cha mgonjwa.
Ghafla  nilisikia ukimya ukitawala  na ile sauti ya mikoromo  niliyoisikia mwanzoni haikuwepo tena ! mmh! Kuna jambo!   nikajiuliza he! Ina maana bi mkubwa amefariki?  Maskini!  Rooho iliniuma sana ingawa sikuwahi kuiona hata sura yake.
Nesi alikuja na kumshughulikia Yule bi mkubwa na wakamtoa na kumpeleka panapo husika wodi ya mwisho hospitalini inayoitwa mortuary.  Wodi ambayo kila nafsi itaingia  hata ukiwa mjanja vipi? 

kawaida ya ukarimu wa watanzania muda wa kazi ulipoisha wafanyakazi wenzie Anita walikuja hospitali kuniangalia mama wa mfanyakazi mwenzao ambao pia walinifahamu, kiukweli nani asiyenifahamu Mama Mjata mie?
Mmoja wapo wa wafanyakazi hao alimwona nesi Yule aliemhamisha bi mkubwa wodini aliyefariki wakamwomba ili awape ruhusa waweze kuniona  kwa vile muda ulikuwa bado kidogo wa kuruhusiwa kuona wagonjwa.
“mama nesi tunaomba tukamwone mama wa mfanyakazi mwenzetu mwl. Mhina amelazwa hapa”
Nesi bila ya kuwaza mara mbili  akatamka  “aah!  Mbona yule mama amefariki”
Wakastuka wote na kutaka kujua zaidi kuhusu kifo na nesi aliwahakikishia kuwa ni kweli amefariki na wametoka kumpeleka mourtuary sasa hivi.
 Mwenye kulia alilia mwenye presha ilipanda ili mradi kila mwenye kuupokea msiba kwa staili yake aliupokea lakini mwisho walipeana moyo wakafuta machozi na safari ya kwenda kwa Anita ilianza.

Huku ndani wodini mimi nimekaa njaa sasa inanikwangua sana, nikafikiria kumwomba nesi akaninunulie walau chips lakini nikajitia moyo kuwa mwanangu si analeta chakula ntakula tu. mfano nikinunua chips, nikala, nkashiba yeye akija na chakula halafu akaona sili si atajisikia vibaya? na nitakuwa kama nimemsumbua bure.... ngoja tu nijikaze,  nilijiwazia peke yangu. 
Lakini pia wasiwasi ukaanza kunishika.... mbona anita ametumia muda mwingi sana toka alipotoka hapa nikizingatia kuwa sio mbali kutoka hospitali na nyumbani kwake? au kuna lolote limemkuta? Au kapata ajali kwa vile anatumia usafiri wa bodaboda? Nikaanza kujitisha inawezekana kapata ajali? Ndio atakuwa amepata ajali maana haiwezekani kuchelewa hivi.
Wafanyakazi wanaofanya kazi na Anita walifika nyumbani na kumkuta Anita yuko busy anamalizia kufunga chakula ili arudi hospitali huku akionekana wazi hana habari za kifo cha mama yake mpenzi. Wakaangaliana na kukosa la kusema, maana walitegemea watakuta kilio au walau vitu vimeshatolewa nje na pilika za maandalizi ya msiba yanaendelea lakini haikuwa hivyo wakaangaliana na mmoja akajitia moyo na kutamka.
“Anita lete hicho chakula sisi tupeleke wewe baki hapa upumzike maana utakuwa umechoka sana”
Kabla anita hajapata nafasi ya kujibu chakula kilishachukuliwa na mchukuaji kisha ondoka nacho. Wengine wakajikaza lakini msiba ni msiba huwezi kujikaza lazima mmoja atashindwa kuzuia machozi yake ikabidi wamkalishe mfiwa chini na kumweleza kilichotokaea kwamba mama hatunae tena duniani!
Wewe hukuwepo lakini malaika wako alikuwepo Anita kwanza alistuka pili hakuamini tatu hakuelewa kwa mara moja inakuwaje?  Kwa homa ile ile? Au presha au? Mama yangu mimi kaitoka?  kilio kilipamba moto na ndipo hakukuwa na siri tena ila ni kweli mama amefariki ndipo sasa msiba ukaanza kukusanya watu na majirani,wenye kumlilia mama, bibi, mwalimu, msanii mashuhuri, shangazi ili mradi ikawa mtafaruku kilio kimepamba moto.  Kumbuka hapa ni bagamoyo hivyo mara moja simu ikapigwa dar na Tanga na Tanzania nzima pia  habari zikafika chuo cha sanaa bagamoyo (tasuba) na raisi wa wasanii chuoni hapo akaziweka kwenye mtandao na huko dare s salaam akina natasha na caftany wakazipata pamoja na wasanii wengine na ghafla R.I.P. zikaanza kutupiwa kwenye mtandao kwa fujo kila mmoja akijaribu kuonyesha upendo  wake kwa marehemu.
Wodini mimi njaa inazidi kukwangua na woga nao ukinitawala mbona Anita amechelewa itakuwa ni ajali tu na kwa vile simu ilizima na sikuona sababu ya kuichaji maana ni mgonjwa itanisumbua tu kumbe huko nje watu wanapiga simu yangu na wanapoona haikuwa hewani wanajua hakika nimekufa.
Ndugu wa dar wakatafuta usafiri na kuanza safari ya kuja bagamoyo msibani.
Jambo limezua jambo!
Mchungaji na wasaidizi wake ambao wana ruhusa ya kuingia wodini muda wowote alikuja akiwa katika ratiba yake ya kawaida huku akiwa ameshapata habari za msiba kwa vile ananifahamu  na huwa tunasali pamoja akawa anapita kuwaombea wagonjwa labda akiwa na mawazo akimaliza ratiba yake hapa ndio aende msibani, katika pitaptia yake akaniona akastuka kidogo ila kwa vile ni mchungaji akajikaza  na kuja kunisalimia  na tukafanya maombi pamoja na alipomaliza akaondoka akiwa amepoteza uchangamfu wake wa kawaida.
Mchungaji alienda moja kwa moja msibani na kukuta watu wako busy na kilio.mchungaji akaamua kuwanyamazisha bila mafanikio.
“amani iwe kwenu”  vilio villiendelea .
Ikabidi atumie nguvu ya ziada na kuwanyamazisha na waliponyamaza akawaambia ukweli ulivyo kuwa mama hajafa ni mzima wa afya hospitalini, habari zikaanza tena kuvuma kuwa badala ya rest in peace sasa ni live in peace na badala ya machozi ya kilio sasa yakageuka machozi ya furaha!
Rais wa wasanii bagamoyo tasuba akamtuma mwalimu hospitali kuja kuthibitisha na  aliniona na nikaongea nae ingawa haya yote yanafanyika hakuna mtu alieniambia chochote hivyo mimi sikuwa najua kama nimekufa na kufufuka na kila anaekuja ingawa anastuka lakini hawaniambi  ingawa nilishangazwa na hali iliyojitokeza ghafla watu wakaanza kuja wodini wanachungulia madirishani wakiniangalia mimi nikadhania  kwa vile ni staa kama kawaida ya wapenzi wetu huwa wanafurahi kuniona kumbe wenzangu walikuwa wanashang’aa mimi kuwepo hai.  mwalimu wa chuo alietumwa alipopata uhakika  akarudi chuo na kumwambia rais wa wasanii tasuba na akabadilisha tangazo la kifo mtandaoni .
Usiniulize wale waliokuwa njiani wakitoka dar kuja msibani bagamoyo maana walifika kweli, mkanganyiko uliotokea tanga na Tanzania nzima kwa wale wanaonifahamu  utajaza mwenyewe.
Swali ambalo wengi walijiuliza ilikuwaje mpaka haya yote yakatokea?
Kwanini nesi ajibu kuwa nimekufa wakati niko hai?
Ni kweli nesi hakuwajibika  na alikurupuka?
Sikiliza nikwambie kilichotokea mpaka hali ikafikia hapa ilipofika 
Nililazwa hospitali nikiwa nasumbuliwa na malaria na simu yangu ilikuwa haina chaji nikaizima na sikuiwasha tena, hili lilikuwa jipu la kwanza.
Mimi naitwa mama mjata na mwanagu anaitwa  Anita au mwl. Mhina na Yule bi mkubwa aliefariki anaitwa ne Mhina.
Kwahiyo kwa lugha nyepesi unaweza sema mama mzazi wa mwl.Mhina anaitwa ne mhina!  Nesi akaunganisha! Simple as that!  Lakini hakujua kuwa kosa alilofanya liliathiri taifa zima!
Na hili  linaweza kuwa jipu letu wote sio nesi peke yake ila watanzania wote. TUTAFAKARI KABLA YA KUTAMKA CHOCHOTE.  ULIMI NI KITU KIDOGO LAKINI KINAWEZA KUSABABISHA BARAKA,LAANA AU MAUAJI YA KIMBARI.
 

Habari hii imeandikwa na Susan Natasha Humba kwa niaba ya mama mjata alienihadhithia mwenyewe.
Nina mshukuru Mungu kwa ajili ya mama Mjata ni mama mwema, mpole na muelewa na tumepewa tena huyu mama na Mungu ili tuendelee kuchota hekima na Baraka zake, nakuombea uishi zaidi na zaidi ili jina la bwana lizidi kubarikiwa kupitia wewe.

Chapisha Maoni

Please Select Embedded Mode To Show The Comment System.*

Mpya zaidi Nzee zaidi