Mahesh Babu na Priyanka Chopra kuja nchini, kushuti Serengeti

Na Mwandishi Wetu

Mtengeneza filamu Maarufu nchini India (Bollywood) S.S. Rajamouli, anatarajiwa kuanza ratiba mpya ya kushuti filamu yake inayosubiriwa kwa hamu kubwa ya SSMB 29, yenye mastaa wa kimataifa Mahesh Babu na Priyanka Chopra.

Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, kikosi kazi kitatia kambi na kuanza kurekodi filamu hiyo ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Tanzania, kuanzia mwishoni mwa mwezi Julai, mwaka huu kwa bajeti ya kufikia TZS bilioni 306.

Filamu hiyo pia inamshirikisha muigizaji maarufu kutoka Malayalam, Prithviraj Sukumaran, na inaelezwa kuwa ni mchanganyiko wa vituko, historia ya kale na mafumbo ya kiutamaduni, ikivutia simulizi za zamani za asili ya kiafrika.

Gazeti la burudani la India Eastern Eye limeripoti kuwa gumzo kuhusu filamu hiyo ya SSMB 29 limeongezeka zaidi baada ya gazeti la Tanzania la The Citizen kuthibitisha uwepo wa ‘shooting’ ya filamu hiyo huko Serengeti

Kwa mujibu wa vyanzo vya karibu, filamu hiyo inahusu mtafiti jasiri anayeanza safari hatarishi kupitia maeneo ambayo hayajachunguzwa barani Afrika.

Filamu hiyo, iliyopata msukumo kutoka kwa filamu maarufu kama *Indiana Jones*, inamuonesha mhusika mkuu akikabiliana na mazingira hatari, masimulizi ya kale ya wenyeji na adui mwenye nguvu, huku akifukua siri iliyosahaulika ambayo inaweza kubadili hatima ya dunia.

Mahesh Babu anatarajiwa kuigiza mhusika mkuu kwenye filamu hiyo, jukumu ambalo linadhaniwa kuwa gumu zaidi kwake ukilinganishwa na kazi zake mbalimbali alizofanyaga.

Priyanka Chopra, ambaye amerudi kwenye tasnia ya filamu za India baada ya kupambana Holywood kwa muda mrefu, atakuwa na nafasi muhimu katika filamu hiyo.

Licha ya Serengeti kuwa eneo kuu la upigaji wa awamu hii ya filamu, timu hiyo inatarajiwa kuhamia Afrika Kusini kwa picha za ziada.

Ripoti za awali pia zilieleza kwamba filamu hiyo itakuwa na kiini cha kihistoria na kiutamaduni kinachotokana na masimulizi ya India, hivyo kuiweka filamu hiyo katika daraja la kipekee kati ya tamaduni za Afrika na Asia.

kushutiwa kwa *SSMB 29* nchini Tanzania si tu tukio kubwa la kimataifa kwenye tasnia ya Filamu, bali pia ni fursa ya kuitangaza nchi kama kitovu cha kuvutia kwa waandaaji wa filamu duniani.

Kwa kuhusisha jina kubwa kama Rajamouli na waigizaji wa hadhi ya kimataifa, wadau wa sekta ya filamu wanatabiri kuwa SSMB 29 huenda ikawa miongoni mwa kazi kubwa zaidi za sinema ya India kuwahi kutokea.

Chapisha Maoni

Please Select Embedded Mode To Show The Comment System.*

Mpya zaidi Nzee zaidi