Na Mwandishi wetu
Mwenyekiti wa Kamati ya Tuzo za Filamu za Moffa, Ndugu Ramadhani Bigale, amekutana na Kaimu Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania (BFT), Dkt. Gervace Kasiga, kujadili kuhusu maandalizi ya tamasha la tuzo za filamu zinazotarajiwa kufanyika mkoani Morogoro.
Kwenye mazungumzo yao, Ndugu Bigale alimhakikishia Dk. Kasiga kuwa kwa mwaka huu, tamasha hilo litakuwa kubwa zaidi kwa kuwa linaandaliwa kwa ushirikiano wa mikoa minne. Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa tuzo za aina hii kushirikisha mikoa mingine, jambo ambalo linatarajiwa kuongeza ubora na ushindani wa filamu zinazoshindanishwa
Aidha, Mwenyekiti wa kamati, Ndugu Ramadhani, alifafanua hatua mbalimbali za maandalizi ambazo tayari zimeshachukuliwa ili kuhakikisha kuwa matukio yanaendelea vizuri na kufanikiwa kikamilifu.
Kwa upande wake, Dk. Gervace Kasiga alitolea wito wa ushirikiano kutoka kwa Bodi yake.
Alimhakikishia Ndugu Bigale kuwa Ofisi ya Katibu Mtendaji iko tayari kutoa msaada wowote ule unaohitajika, na kuahidi kuwa Bodi ya Filamu Tanzania wanaunga mkono kamati nzima ili tuzo za mwaka huu ziwe na kiwango cha hali ya juu kuliko kawaida na kukidhi matarajio ya wadau na wakazi wa Morogoro.
Pamoja na kauli ya ushirikiano huo, Dk. Kasiga alisisitiza umuhimu wa kamati hiyo kushikamana na misingi na taratibu zilizowekwa na serikali kupitia BFT kuhusu utoaji na uendeshaji wa tuzo za filamu nchini.
Akiongezea, aliwasihi kamati hiyo kutumia majaji wenye sifa na uzoefu mkubwa wa kitaaluma katika fani ya filamu na ujuzi wa kutosha ili kuhakikisha uchaguzi wa washindi ni wa haki, na unaoakisi ubora halisi.
